Habari

Je! Ungependa wafanyakazi wako wakupende? Fanya Haya

Kila mtu anapenda watu wamthamini na wampende, vivyo hivyo hata kwa mabosi  wanahitaji kupendwa na kuthaminiwa maeneo ya kazi, ingawa kama mabosi huwa hawatambui kama wao ni mabosi wabaya. Dondoo hizi chache zitakupa mwangaza wa mambo ambayo yatakufanya ujenge uhusiano bora na wafanyakazi wako na kuongeza utendaji kazi wenye manufuaa kwa biashara yako na ofisi yako.

557487_524184147615607_2095366320_n
Picha na Gavin Gosbert (Black n While Visual Studios)

Kitu cha kwanza kabisa , wewe kama bosi usiwe mrusha lawama kwa wafanyakazi wako
Kama vile unavyopenda uthaminiwe hata wafanyakazi wanapenda wafanyiwe hivyo, unatakiwa kuwashauri na kwenda nao kwa utaratibu mzuri ili kazi zifanyike vizuri na uhusiano wenu wa kazini na hata maeneo nje ya kazi yaendelee kuwa mazuri. Hii itakusaidia hata ukiwa nje ya eneo la kazi kupata msaada mzuri kwa kuwa unathamini watu wengine.

Weka matarajio yako waziwazi
Kiongozi mzuri huyaweka matarajio yake wazi kwa watu anaowaongoza, wajulishe unaowaongoza ni kitu gani unakitarajia kutoka kwao na kwa kiwango gani. Unahitaji kuwa muwazi kwa kila kitu kinachohusu kazi  na majukumu katika kitengo chako.

Uwe mwenye msimamo wa kusimamia ulichokisema
Je umesema nini kuhusu mipango ya mwaka huu? Je uko tayari kusimamia maneno yako mwenyewe uliyoyasema kwa wa tu unaowaongoza? wafanyakazi wengi hawapendi mabosi vigeugeu, wanapenda watu wanaotekeleza walichokisema wenyewe.

Toa Mrejesho
Wewe kama bosi unahitaji kutoa mrejesho wa kila kitu ambacho wafanyakazi wamekuwa wakifanya ili watiwe moyo na kuonyesha kuwa wanathaminiwa katika mchango wao. Usitoe mrejesho pale tu mambo yameenda vibaya onyesha kuthamini mchango wao kwa kila kitu. Waambie pale ambapo walifanya vizuri na pale ambapo mambo hayakwenda vizuri na namna ya kuboresha ikiwezekana wasaidie namna ya kuboresha kama muda haukutosha au vitendea kazi vilikuwa pungufu wewe ni sehemu yao na wao ni sehemu yako itakayoonyesha kufanikiwa au kutofanikiwa.

Unatakiwa kuwa muwazi katika masuala ya utendaji na utekelezaji wa kazi, unahitaji kuwajulisha maeneo ya kurekebisha na namna ya kurekebisha. Kama utakuwa ukiwalalamikia walio chini yako na wao hawajui unacholalamikia, tatizo lipo kwako. Vile vile omba au kuuliza mambo ya kurekebisha kwa wafanyakazi unaowaamini. Weka mazingira ambayo wafanyakazi hawataogopa kutoa ushauri au kukushauri kuhusu jambo hilo linaweza kuchukua muda gani kufanyika kwa usahihi.

Zingatia matokeo zaidi.
Hata kama una sheria na taratibu hakikisha zina uhusiano na kile mnachokifanya na kufikia malengo mnayoyahitaji. Uwe tayari kulegeza masharti na kanuni kuliko kuangalia sana masharti na ukakosa kufikia malengo yanayohitajika. Usiwe mtu mtata sana.

Unatakiwa kujua vitu vinafanyikaje na ujifunze namna ya kufanya
Usiwe ni mtu wa kutaka kitu kifanyike kwa namna fulani halafu wewe mwenyewe hujui kuhusu ufanyaji wa hicho kitu. hii itakusaidia kuangalia namna ya kufanya, kusaidia au kuongeza nguvu kazi.

Punguza usanii kazini
Kama kitengo chako kina visa vingi kupitia kwa wafanyakazi wako, umbea na maneno ya chini chini inamaanisha hufanyi kazi sawasawa. Weka taratibu za maisha hapo kazini ikiwa  ni utani uwe kwa namna gani na tamaduni za ofisi ni zipi.

Wasaidie wafanyakazi kujua vitu gani vitaboresha utendaji wao na wavipate.
Hii inaweza kuwa ni mafunzo, namna ya kuboresha uhusiano kazini, teknolojia ya mawasiliano na habari na namna ya kuongeza ufanisi.

Usiogepe kufanya maamuzi magumu
Kazi yako ni kutatua matatizo na sio kukimbia matatizo. Hivyo kuna wakati utaingia kwenye mjadala mzito na mgumu kitu kinachokupelekea kufanya maamuzi yasiyotegemewa sana na watu wengine kutoka kwako.Usiogope kuwakwaza wafanyakazi  weka taratibu na madhara ya kutofuata hizo taratibu. Fanya maamuzi magumu.

Fanya kazi na watu kwa Upendo na kuwathamini
Hata kama ni wakati mgumu au mnapitia wakati mgumu onyesha upendo na kuwathamini watu. Wewe ndo mwenye nguvu na mamlaka katika eneo hili la kazi una wajibu na jukumu la kuonyesha utu na uthamani wa kila mfanyakazi.  Washukuru watu wanaofanya kazi pamoja na wewe,wajibu wafanyakazi wako vizuri na kwa utu, wasaidie kujifunza na kujua mambo kwa utaratibu na mawazo mazuri.

Awali Mwaisanila

A Personal Career Development specialist, passionate about empowering emerging generations of student, graduates and working class.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents