Kikosi cha PSG chakwama ndani ya lifti Ujerumani
Wachezaji 11 wa kikosi cha PSG walikwama kwa zaidi ya dakika 50 ndani ya lifti wakati wakitoka kwenye hoteli waliyofikia nchini Ujerumani wakielekea katika maandalizi yao ya mchezo wa Champions League dhidi ya wenyeji RB Leipzig.
Tukio hilo limetokea siku ya Jumanne wakati nyota 11 wa PSG wakitoka kwenye hoteli waliyofikia wakielekea katika maandalizi ya mechi hiyo iliyopigwa usiku wa Jumatano na kushuhudia Paris Saint-Germain Football Club ikipigwa kwa jumla ya magoli 2 – 1 dhidi ya wenyeji RB Leipzig.
Kwa mujibu wa Le Parisien, kundi kubwa la wachezaji walikwama katika lifti zaidi ya dakika 50 na kuokolewa na ‘firefighters’. Beki wa PSG, Layvin Kurzawa aliposti klip katika Instagram inayowaonesha ‘firefighters’ wakijaribu kuwanasua.
Hata hivyo baadaye alifutiliambali kipande hiko cha video licha ya kuwa ameshachelewa kwa kuwa mashabiki wengi walikuwa wameshaanza kutumiana kupitia mitandao ya kijamii.
Taarifa kutoka Ufaransa zinadai, Kurzawa alikwama na wenzake Presnel Kimpembe, Leandro Paredes, Angel Di Maria, Marquinhos, Bandiougou Fadiga, Abdou Diallo, Idrissa Gueye, Moise Kean, Colin Dagba na Kays Ruiz-Atil.