‘Neymar Judgement Day’: Rais wa Barcelona, wajumbe wa bodi kumfuata Neymar na mkwanja mkononi + Dembele
Wajumbe wa bodi ya Barcelona kwa mara nyingine tena wanasafiri kwenda Paris kujaribu kukamilisha dili ama mpango wa kumrudisha Neymar huko Nou Camp.
Rais wa klabu ya Barcelona, Josep Bartomeu pamoja na mkurugenzi wake, Eric Abidal wamesafiri kueleke makao makuu ya klabu ya Paris Saint-Germain hii leo siku ya Jumanne.
Miamba hiyo ya La Liga wanapambana kufa na kupona ili kuhakikisha wanamrejesha Mbrazil huyo ndani ya timu ya Barcelona na wamemuandalia dau la mwisho.
Barcelona tayari wamemuandalia Neymar dau la dola za Kimarekani milioni 155 kwa msimu ujao wa usajili huku mipango iliyopo kwa sasa ni kumng’oa kwa mkopo ili kuepukana na rungu la FIFA kuhusu matumizi makubwa ya fedha za usajili baada ya kumvuta Griezmann.
PSG walikataa ofa hiyo na kwa sasa wanasubiria dili la euro milioni 100 ambalo litajumuisha pamoja na wachezaji Ousmane Dembele na Nelson Semedo.
Mabingwa hao wa Ufaransa wanaamini hiyo ingekuwa njia rahisi yakumwachia Neymar lakini kwa Barcelona imekuwa ngumu kuwaachia wachezaji wake wawili wa kikosi cha kwanza.