Rais Samia awanyooshea kidole wanaobeza jitihada za serikali
Rais Samia Suluhu Hassan amesema nchi lazima ikope ili kuendeleza miradi mikubwa ya maendeleo, na tayari mifuko na wafadhili kadhaa wamekubali kuipa nchi zaidi ya shilingi trilioni 7 kwa ajili ya kutekeleza miradi hiyo.
Akizungumza Ikulu jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya kupokea taarifa ya Matumizi ya Fedha za Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO -19, Rais Samia Suluhu Hassan amesema mikopo ni lazima na tozo zitaendelea ili kuwaletea Wananchi maendeleo.
Amesema jambo linaloisukuma Serikali yake kukopa ni kuendeleza maendeleo ya watu, na Tanzania itakopa mikopo yenye riba nafuu na itakuwa makini na mikopo inayochukua.
Kuhusu madeni ya nchi Rais amesema, Serikali italipa madeni yaliyoiva ili kutoa fursa kwa Tanzania kulipa madeni mengine na kutoa huduma kwa Watanzania.
Kuhusu baadhi ya watu wanaolalamika juu ya Serikali yake kukopa Rais amesema, hataacha kukopa kwa maendeleo ya Watanzania na hatakuwa Rais wa kwanza kukopa kwa ajili ya Watanzania.
Source: TBC