Habari

Taarifa kuhusu kondomu milioni 500 zinazotarajiwa kusambazwa nchini

Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imetoa ufafanuzi kuhusu taarifa ya serikali kusambaza kondom 500,000,000 katika kipindi cha miaka mitatu 2018 hadi 2020. Taarifa iliyotolewa na katibu wa wizara hiyo imeeleza kuwa Kumekuwa na taarifa mbalimbali, hamaki na kejeli zinazoenea katika mitandao ya kijamii kuhusiana na taarifa iliyotolewa tarehe 27 Novemba 2017, Mnazi Mmoja kwenye uzinduzi wa Mkakati wa Taifa wa Kondom kuhusu mpango huo wa Serikali.

Tunapenda kuukumbusha umma wa Watanzania kwamba matumizi ya kondom ni moja wapo ya afua katika kuzuia maambukizi mapya. Hata hivyo utafiti wa viashiria vya Malaria na UKIMWI wa mwaka 2011/12 umebaini kuwa kuna matumizi duni ya kondom, kwani ni asilimia 27 tu ya watu wenye wenza zaidi ya mmoja waliokiri kutumia kondom mara ya mwisho walipofanya ngono. Hivyo Serikali itaendelea kununua na kusambaza kondom kwa lengo la kuzuia maambukizi ya VVU, magonjwa ya ngono na mimba zisizo tarajiwa ikiwa ni mojawapo ya afua hizo za kudhibiti maambukizi ya VVU.

Hivi sasa nchini kuna vyanzo vya upatikanaji wa kondom vya aina tatu. Kwanza ni kondom zinazopatikana kupitia sekta ya umma  ambazo husambazwa na Serikali kwa wananchi bila malipo. Pili, kuna kondom zinazosambazwa na wadau ambazo zinauzwa kwa bei ya chini kwa kuwa wadau wamechangia. Mfano kondom za Salama na Dume, na chanzo cha tatu ni kondom za kibiashara ambazo zinauzwa kwa bei ya kati na ya juu. Kondom za sekta ya umma husambazwa kupitia vituo vya kutolea huduma za afya na huduma za mkoba ngazi ya jamii, Kondom za wadau na zile za biashara husambazwa katika maduka ya dawa, maduka ya bidhaa mbambali, baa na nyumba za wageni.

Kwa mwaka 2016/17 Serikali iliboresha kondom zinazopatikana kupitia ya sekta ya umma kwa kuipa kifungashio kipya na jina la ZANA, ambapo kondom 36,916,911 zilisambazwa. Kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia 2018 hadi 2020 Serikali kwa kushirikiana na Mfuko wa Dunia wa kudhibiti malaria, UKIMWI na Kifua Kikuu inatarajia kununua kondom za kiume takribani 500,000,000. Kondom hizi zitasambazwa kupitia vituo vya kutolea huduma za afya na katika maeneo hatarishi yanayoaminika kuwa na watumiaji wengi.

Aidha ikumbukwe kwamba nchi yetu ina sera sheria, mila, desturi na maadili yetu kama watanzania,  Hivyo kondom zote haziruhusiwi kusambazwa bila kufuata miongozo ya Wizara, ili kulinda zisifike kwa wasiolengwa.

Hivyo basi, iwapo tunataka kuzuia na kumaliza maambukizi ya VVU na UKIMWI ifikapo 2030 tunapaswa kama nchi kuwekeza katika kuzuia maambukizi mapya. Matumizi ya kondom, ununuzi wa vifaa tiba, vitendanishi, dawa za ARV na za magonjwa nyemelezi ni afua muhimu. Tunaomba wanahabari na wananchi waunge mkono juhudi hizi kwa kuwa tunahitaji watanzania wenye afya bora na uwezo wa kuzalisha ili kuijenga Tanzania ya Viwanda.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents