Daz Baba: Msiamini yaliyoandikwa, mimi nipo fit
Daz Baba amedai kuwa yupo gado kama Zay B tofauti na magazeti ya udaku yalivyoandika miezi ya hivi karibuni. Baada ya kukaa kimya kwa muda mrefu, msanii huyo amesema anajiandaa kuja na album yake mpya.
Daz Baba ameiambia Bongo5, kuachia kwake album kutawafanya mashabiki wake wapate kazi zake kwa wingi tofauti na kuachia single moja moja.
“Unajua watu wameshazusha mengi kuhusu maisha yangu lakini ninachosema kwa mashabiki wangu mimi nipo njema na harakati za muziki zinaendelea kama kawaida,” alisema.
“Nipo kwenye mchakato wa kuachia album yangu mpya ambayo nitauza mimi mwenyewe bila kutegemea mhindi. Unajua hii ni biashara kama biashara nyingine inategemea unajipanga vipi ili ufanye biashara.”
Pia Daz amewataka mashabiki wake kusikiliza wimbo wake mpya uitwao ‘Pointer’ pamoja na kukaa tayari kwa ujio wa video mpya na kazi mpya akiwa na Juma Nature.