Habari

Kigoma: Naibu Waziri wa afya ashiriki ujenzi wa shule

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto,Dkt. Faustine Ndugulile ameshiriki ujenzi wa Shule ya Kijiji cha Nyanganga iliyoko kata ya Kazuramimba, wilaya ya Uvinza mkoani Kigoma ikiwa ni jitihada za wananchi wa kijiji hicho kuharakisha upatikanaji wa huduma ya elimu kijijini hapo.

Akiwa katika Kijiji hicho Naibu Waziri Dkt. Ndugulile ameshiriki zoezi la kumimina zege kwa ajili ya kufunga ‘rental’ ya vyumba vya madarasa ya shule hiyo.

Dkt. Ndugulile amesema lengo la kuwepo ziara hiyo ni kufuatilia utekelezaji wa Sera ya Maendeleo ya Jamii (1996), na Sera nyingine za Wizara amabzo zinasisitiza ushiriki wa jamii katika kuibua mahitaji, kupanga, kuamua, kutekeleza, kufuatilia na utathmini shughuli za miradi ya maendeleo ikiwemo uboreshaji wa huduma ya miundo mbinu ya kufundishia na kujifunzia katika maeneo ya mijini na vijijini.

Mhe. Ndugulile ameongeza kuwa Ili kurejesha ari ya wananchi kushiriki katika maendeleo yao kuelekea uchumi wa kati na wa viwanda, Wizara imeamua kufuatilia utekelezaji wa Sera ya Maendeleo ya Jamii katika ngazi za Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa kuhamasisha jamii kushiriki na kuchangia shughuli za maendeleo yao kwa kufanya kazi za bega kwa bega, kuchangia nguvu zao, rasilimali fedha, rasilimali vifaa na ufundi kwenye utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa miundo ya elimu, afya, kilimo, mifugo, barabara na viwanda vidogo vidogo.

“Nimeambiwa kuwa mradi wenu wa ujenzi wa shule ya sekondari katika kijiji cha Nyanganga utasaidia kusogeza huduma ya elimu jirani na wananchi, na nimevutiwa na hamasa mliyonayo katika maendeleo na nimekuja kushirikiana nanyi kuendeleza ujenzi wa madarasa ya shule kazi ambayo ni kigezo thabiti cha cha dhamira ya dhati yawananachi wa kijiji hiki katika kutoa haki ya msingi ya kumwendeleza Mtoto katika ngazi ya kijiji na jamii kwa ujumla” alisisitiza Mhe. Dkt. Ndugulile.

Kwa upande wake Mtendaji wa Kjjiji cha Nyanganga Bw.Erick Ruhomola amesema kuwa Mradi wa ujenzi wa Shule ya Sekondari ya kijiji uliibuliwa na kubainishwa na wananchi wenyewe na kutekelezwa na wananchi kwa takribani asilimia mia moja hadi kufikia hatua ya kumwaga zege kwa ajili ya ‘rental’.

“Tunaishukuru Serikali kwa kutuona na kuja kutuunga mkono katika jitihada zetu za kujiletea maendeleo katika kijiji chetu” alisisitiza Bw. Ruhomola.

Naye Mkuu wa Wilaya yaUvinza Mhe. Mwanamvua Mrindiko amemshukuru Naibu Waziri kwa kuja kuonesha mfano wa kuamsha ari ya wananchi wa Uvinza kujitolea katika shughuli za maendeleo yao.

“Hili ni Jambo la kipekee kwa Mhe. Naibu Waziri kutembelea na kushiriki na wananchi katika ujenzi wa shule hii” alisisitiza Mhe.Mwnanamvua

Ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Kijiji cha Nyanganga kilichopo Wilaya ya Uvinza Mkoa wa Kigoma itawasaidia watoto wa jamii hiyo kuwa na shule karibu na makazi yao ambapo hapo awali watoto hao walikuwa wanatembea umbali wa kilometa 14 kwenda shule ya jirani.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile yupo katika Mkoa wa Kigoma kwa ziara ya siku mbili ya kikazi kufuatilia utekelezaji wa Sera mbalimbali zinazosimamiwa na Wizara yake.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents