Mahujaji 60,000 pekee washiriki Hijja mwaka huu
Mahujaji Jumapili waliondoka kwenye mji mtakatifu wa Mecca nchini Saudi Arabia kuelekea Mina ikiwa kama sehemu ya ibada ya hijja ambayo kwa mwaka wa pili sasa inahudhuriwa na watu wachache kutokana na janga la Corona.
Kwa mujibu wa shirika la habari la AFP ,ni watu 60,000 waliopokea chanjo kamili kutoka nchini humo, ambao wameruhusiwa kushiriki.
Katika nyakati za kawaida, takriban mahujaji milioni 2.5 hushiriki. Tangu Jumamosi makundi ya mahujaji yamekuwa yakifanya Tawaf kwenye msikiti mkuu wa Mecca wakati wakizunguka kwenye Kaaba.
Baada ya hatua hiyo mahujaji huelekea Mina ambalo ni bonde linalozungukwa na milima takriban kilomita 5 kutoka msikiti mkuu wa Mecca. Mahujaji waliletwa Mecca Jumapili kwa mabasi yaliokuwa na watu wachache tu kutokana na kanuni za kujiepusha na maambukizi ya corona.
Serikali imesema kuwa imeweka walinzi kutoka makampuni ya kibinafsi kwenye maeneo ya umma ili kuhakikisha kuwa watu wanaweka umbali unaohitajika ili kujiepusha na maambukizi.
By-BAKARI WAZIRI