Samatta na Victor Wanyama watemwa na CAF
Shirikisho la soka barani Afrika (CAF) limetaja majina matano ya wachezaji watakaowania tuzo ya mchezaji bora wa Afrika kwa mwaka 2016.
Wachezaji waliotajwa kuwania tuzo hiyo ni pamoja na Pierre-Emerick Aubameyang wa Borrusia Dortmund (Gabon), Riyad Mahrez wa Leicester (Algeria), Sadio Mane wa Liverpool (Senegal), Mohamed Salah wa Roma (Misri) na Islam Slimani wa Leicester (Algeria).
Awali CAF ilitangaza majina 30 ya wachezaji watakaowania tuzo hiyo huku Mbwana Samatta pamoja na Victor Wanyama wa klabu ya Tottenham, Yannick Bolasie wa DR Congo anayechezea Everton na wengine walikuwa ni miongoni kati ya wachezaji waliotajwa kuwania tuzo hiyo.
Wachezaji wengine waliotajwa kuwania tuzo ya mchezaji bora wa Afrika kwa wanaocheza ligi za Afrika ni pamoja na Khama Billiat wa Mamelodi Sundowns (Zimbabwe), Keegan Dolly wa Mamelodi Sundowns (South Africa), Rainford Kalaba wa TP Mazembe (Zambia), Hlompho Kekana wa Mamelodi Sundowns (South Africa) na Denis Onyango wa Mamelodi Sundowns (Uganda).
Tuzo hizo zitatolewa Alhamisi ya Januari 5 mwakani mjini Abuja, Nigeria.