Mbunge wa CHADEMA kupendekeza muda wa Rais madarakani upunguzwe
Mbunge wa Tarime Vijijini kupitia tiketi ya Chadema, Mhe. John Heche amekusudia kuwasilisha bungeni hoja binafsi ya kupunguza muda wa viongozi kukaa madarakani kutoka miaka mitano na hadi minne .
Kauli ya John Heche imekuja zikiwa zimepita siku kadhaa toka Mbunge wa Chemba Mhe. Juma Nkamia (CCM) kusema anatarajia kuwasilisha muswada binafsi bungeni kulitaka bunge kufanya marekebisho ya katiba ili viongozi waweze kukaa miaka saba, Jambo ambalo Heche anapinga na kusema kuwa muda ambao viongozi wanakaa madarakani ni mkubwa sana.
“Nakusudia kuwasilisha bungeni hoja binafsi kupunguza muda wa kukaa madarakani kwa Rais, wabunge na madiwani kutoka miaka 5 mpaka 4 tuwe kama Marekani ili kutoa nafasi kwa wananchi kuwa na maamuzi zaidi kuhusu uendeshaji wa nchi yao,” ameandika John Heche kwenye ukurasa wake wa Facebook huku akisisitiza kuwa kiongozi akikaa muda mrefu madarakani kwa muda mrefu anajisahau.
SOMA ZAIDI – Wananchi waomba Bunge kumuongezea muda Rais Magufuli madarakani
John Heche ni moja ya viongozi wa upinzani ambao walistushwa na maombi ya Mbunge wa Chemba Mhe. Juma Nkamia (CCM) ya kuongeza muda wa Rais madarakani kwa kusema“mwisho mtataka kuondoa ukomo wa madaraka kwenye katiba. Nini kilichowashinda kufanya kwa miaka mitano ambacho unahisi ukipewa saba utafanya?!”.