Burhani wafanya upasuaji Bure
Hospitali ya Burhani ya Jijini Dar es salaam imeanza kutoa huduma ya bure ya upasuaji jicho kwa watoto wagonjwa 100 wenye matatizo hayo ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya kutimiza miaka Mia moja ya kiongozi wa dhehebu la Bohra Dk. Sydena Burnanuddin Saheb.
Akizungumza Jijini Dar es salaam jana, Mkurugenzi wa hospitali hiyo Sheikh Aliasgar Talib, alisema huduma hiyo iliyoanza jana hadi Februari 20 Mwaka huu imelenga kuwasaidia wananchi wenye ukosefu wa kipato ambao kwa namna yoyote wanashindwa kugharamia matibabu hayo.
Alisema huduma hiyo inatolewa kama sehemu ya kusheherekea Miaka Mia moja ya kuzaliwa kwa kiongozi wao na muhasisi wa hospitali hiyo Dk. Saheb, aliyedai kuwa hupenda kuona wananchi wenye matatizo ya kiafya wanasaidiwa matibabu pale inapohitajika.
Alisema katika kuhakikisha wananchi wenye matatizo hayo ya mtoto wa jicho wanapatiwa matibabu kwa uhakika, hospitali hiyo imemleta mtaalam wa matatizo ya macho kutoka nchini India Dk.Mustafa Parekh, atakayefanya matibabu hayo kwa kushirikiana na baadhi ya madaktari waliopo hapa nchini.
Kwa upande wake Mratibu wa huduma ya matibabu hayo Saifuddir Jamal, alisema kabla ya utaratibu wa matibu unatolewa kwa awamu ambapo wagonjwa waliojiandikisha mapema ndio wataanza kupatiwa huduma.
Alisema utaratibu wa kujiandikisha unaendelea kutolewa katika hospitali hiyo pamoja na vituo vilivyopo katika hospitali ya Temeke, Amana na Mnazi mmoja pamoja na hospitalini hapo na kuwataka wananchi wenye matatizo hayo kuwahi kabla huduma hiyo kusitishwa hapo Februari 20 Mwaka huu.
Aidha alisema huduma hiyo imewalenga watu wenye matatizo ya mtoto wa jicho pekee na kwamba hadi jana tayari watu 60 wenye matatizo hayo walikuwa wamechunguzwa matatizo
yao wakisubiri kufanyiwa upasuaji huo.