Road To Mama Yabamba Maisha Club
Ile Pati ya kuelekea kwenye Tuzo za MaMas zinazoandaliwa na kituo chako cha Televisheni ya muziki MTV Base Road To Mamas Party jana usiku ilifanyika katika ukumbi wa disko na burudani za usiku The New Club Maisha.
Pati hiyo ambayo ilikuwa inaitwa Road To Mama Dar-Es-Salaam ilianza kuanzia majira ya saa nne na nusu ambapo kundi la U Dj kutoka Kenya Code Red Djs lilishika mtambo na kuwarusha vilivyo wakazi wa jiji la Dar-Es-Salaam waliojitokeza kuserebuka katika pati ya aina yake.
Pati hiyo ambayo ilifana vya kutosha hasa hasa katika mwonekano na mpangilio wa urembo kuanzia nje hadi ndani ikihusisha zuria jekundu ambalo lilitandikwa maalum kwa wageni wanaowasili pamoja na uwepo wa gari aina ya Hummer 3 ambayo ilipakiwa hapo ikidanganya kama mgeni maalumu sana yupo ndani.
Aidha mpangilio huo haukuishia hapo bali upande wawageni waalikwa wenye umuhimu yaani VIP ulipambwa vilivyo huku matunda, vyakula na vinywaji mchanganyiko vilivyotengenezwa kwa pombe kali na juisi ya matunda pamoja na vitafunwa vidogo vidogo vikipatikana muda wote wa sherehe.
Burudani rasmi ya usiku huo ambayo ndio mzizi wa pati yenyewe ilianza mida ya saa saba na robo usiku ambapo msanii Joh Makini toka Tanzania alikuwa wakwanza kupanda stejini na kuimba nyimbo nne huku akisababishiwa mtamboni na Dj Choka.
Baada ya burudani hiyo ya fungua pazia ilifuta zamu ya msanii wande Coal kutoka Nigeria ambaye naye alipagawisha na vibao vyake vinne kabla ya ma Dj wa Code Red hawajapanda tena mtamboni na kuburudisha mashabiki wa muziki kwa muda wa dakika 30.
Ilifuata zamu ya waganda wawili machachali Moze Radio na Weezle ambao nao kama ilivyo ada yao walipagawisha vilivyo na nyimbo zao nne ambazo ni pamoja na Nakudata, Bread and Butter, VuVuzela na Heart Attack.
Baada ya hapo burudani ilirudi nyumbani na hakuwa zaid ya mtu mwingine bali msanii Diamond ambaye naye pia anawania tuzoza MaMa katika kipengele cha msanii mpya anayechipukia. Msanii huyo alipiga shoo ya nguvu akimbatana na madansa wake wanne waliovalia nadhifu.
Wasanii wa mwisho kutoa burudani katika pati hilo la Road To MaMa Dar-es-Salaam Party walikuwa kundi la P-Unit kutoka Kenya ambao kwa sasa wanatamba na kibao chao Kare. Wasanii hao Gabu, walitingisha vilivyo na vibao vyao vya Kushoto Kulia, Si lazima Hapa Kule na Kare ambayo ilipagawisha vibaya sana.
Pati hiyo ilihudhuriwa na wapenda burudani pamoja na wadau mbali mbali wa muziki kuanzia watangazaji wa vituo vya redio na luninga, wasanii, watayarishaji wa muziki, ma promota na wafanyabiashara mbali mbali wadogo na wakubwa.