Habari

Utawala wa kijeshi Niger wavunja mkataba Kijeshi na Marekani


Kanali Meja Amadou Abdramane
Kanali Meja Amadou Abdramane.

 Utawala wa kijeshi nchini Niger umebatilisha mkataba wa kijeshi ambao uliruhusu kuwepo kwa wanajeshi na wafanyakazi wa kiraia kutoka Wizara ya Ulinzi ya Marekani katika ardhi yake, msemaji wa utawala Kanali Amadou Abdramane amesema Jumamosi.

Molly Phee
Molly Phee

Uamuzi, ambao unaanza mara moja, unafuatia ziara ya maafisa wa Marekani wakiongozwa na Waziri Mdogo wa Mambo ya Nje kwa Masuala ya Afrika Molly Phee na ikimjumuisha Jenerali Michael Langley, kamanda wa Kamandi ya Marekani Afrika.

Abdramane, akiongea kwenye televisheni katika taifa la Afrika Magharibi amesema ujumbe wa Marekani haukufuata taratibu za kidiplomasia na kwamba Niger haikujulishwa kuhusu waliomo ndani ya ujumbe wala tarehe ya kuwasili kwao au ajenda yao.

Ameongezea kwamba majadiliano yao yalihusu mpito wa sasa wa kijeshi nchini Niger, ushirikiano kati ya nchi hizo mbili na maamuzi ya Niger ya washirika katika mapambano dhidi ya wanamgambo wenye uhusiano na al-Qaida na kundi la Islamci State.

Tangu wakamate madaraka mwezi Julai mwaka 2023, utawala wa kijeshi wa Niger, kama walivyo watawala wa kiieshi katika nchi jirani za Mali na Burkina Faso, wameifukuza Ufaransa na majeshi mengine ya Ulaya, na kuigeukia Russia kwa msaada.

“Niger inasikitika kuwa azma ya ujumbe wa Marekani ni kuwanyima watu wa Niger haki ya kuchagua washirika wao na aina ya ushirika wenye uwezo wa kweli wa kusaidia katika mapambano dhidi ya ugaidi,” Abdramane amesema.

“Pia, serikali ya Niger inalaani vikali kwa nguvu tabia ya kujishusha chini inayoambatana na vitisho vya kulipiza kisasi kutoka kwa ujumbe wa Marekani kwa serikali ya Niger na watu,” ameongezea.

Wizara ya Ulinzi ya Marekani haikupatikana kujibu ombi la kutoa maoni.

Kuna kiasi cha wanajeshi 1,100 wa Marekani nchini Niger hadi mwaka jana, ambako Marekani inafanya shughuli za kijeshi kutoka kwenye kambi mbili ikiwemo ya ndege zisizo na rubani inayojulikana kama Air Base 201, iliyojengwa karibu na Agadez katikati mwa Niger iliyogharimu zaidi ya dola milioni 100.

Tangu mwaka 2018 kambi hiyo imetumiwa kuwalenga wanamgambo wa Islamic State na Jama’at Nusrat al-Islam wal Muslimeen (JNMI), mshirika wa al-Qaida, katika eneo la Sahel.

Abdramane amesema hadhi na uwepo wa wanajeshi wa Marekani nchini Niger ni kinyume cha sheria na imekiuka kanuni za kikatiba na demokrasia kwasababu, kwa mujibu wa msemaji, iliamuliwa na upande mmja kwa taifa hilo la Afrika mwaka 2012.

Amesema Niger haikuwa na habari kuhusu idadi ya raia na wanajeshi wa Marekani walio katika ardhi au vifaa vimepelekwa huko na kwa mujibu wa mkataba, jeshi la Marekani halina jukumu la kujibu ombi lolote kwa msaada dhidi ya wanamgambo.

“Kutokana na yote hayo, serikali ya Niger, tunabatilisha haraka sana mkataba unaohusiana na hadhi ya wanajeshi wa Marekani pamoja na wafanyakazi wa kiraia katika Wizara ya Ulinzi ya Marekani kwenye eneo la Jamhuri ya Niger,” Abdramane amesema.

 

 

 

 

 

CHANZO: VOA SWAHILI

 

 

 

Imeandikwa na Mbanga B.

Related Articles

Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents