Nina hasira mahakama haikunitendea haki – Rais Uhuru Kenyatta
Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta ametetea hatua yake ya kuikosoa mahakama ya juu nchini humo na jaji mkuu David Maraga kwa kubatilisha matokeo ya uchaguzi wa urais akisema ni haki yake kufanya hivyo.
Akizungumza katika kampeni za chama cha Jubilee katika kaunti ya Kajiado siku ya jana, Rais Kenyatta amesisitiza kuwa kauli yake kwamba mahakama hiyo ya juu ilipuuza mbali haki ya wananchi ili kumfurahisha mtu mmoja aliyemtaja kuwa mpinzani wake Raila Odinga na kudai kuwa kitendo hicho kimemuongezea hasira ya kurudia uchaguzi kwa nguvu zote.
”Nina hasira kwasababu nilikosewa na mahakama kabisa haikunitendea haki, Walibatilisha uchaguzi wangu kimakosa, lazima tuseme ukweli”, amesema wakati wa kampeni za chama chake katika eneo la Kiserean.
SOMA ZAIDI – Raila Odinga asusia tarehe ya uchaguzi nchini Kenya
Hata hivyo, Bwana Kenyatta akiongozana na naibu wake William Ruto pamoja na viongozi wa chama tawala cha Jubilee, Rais Kenyatta amesema kuwa hakuna kilichobadilika kwa kuwa Wakenya waliompigia kura watampigia kura kwa mara nyingine.
”Tulishinda kwa haki, Tulishinda kwa zaidi ya kura milioni 1.4, lakini mahakama ikaamua kutunyima ushindi wetu, Tuko tayari kwa uchaguzi mpya,”amesema Bwana Kenyatta.