Michezo

Safari ya Hispania ya Farid Mussa yatimia

Mchezaji wa klabu ya Azam FC, Farid Mussa, anatarajia kuondoka nchini kesho Jumatano saa 5.00 usiku kuelekea nchini Hispania kujiunga na timu ya Deportivo Tenerife ya huko.

Farid anaondoka kujiunga na timu hiyo ya Ligi Daraja la Kwanza Hispania kwa mkopo baada ya taratibu zote kukamilika ikiwemo kupata kibali cha kufanya kazi nchini humo.

Akitoa taarifa rasmi ya klabu mbele ya waandishi wa habari, Ofisa Habari wa timu hiyo, Jaffar Idd, alisema kuwa anaondoka baada ya Tenerife kumtumia tiketi ya ndege tayari kabisa kwenda kujiunga nao.

“Mchezaji Farid Mussa kama mnavyokumbuka tuliwaambia taratibu zake zinakwenda vizuri baada ya kukamilisha taratibu zote ubalozini, tunavyoongea na nyinyi hivi sasa ni kwamba klabu ya Tenerife imetuma tiketi ya Farid Mussa na anatarajia kuondoka kesho saa 5 usiku na ndege ya Shirika la KLM, atatoka Dar es Salaam, atapitia Amsterdam, Barcelona na baadaye Tenerife,” alisema.

Idd alisema Azam FC inamtakia kila la kheri winga huyo katika safari yake mpya ya maisha soka huko aendako.

“Kwanza tunamtakia kila la kheri, acheze kwa mafanikio na kuonyesha uwezo mkubwa ili iwe ni sehemu ya kufungua milango kwa wachezaji wengine kutoka Azam FC au klabu nyingine yoyote ya Tanzania,” alisema.

Related Articles

Check Also
Close
Back to top button

Adblock Detected

Please don't block our ads, we rely on these ads to serve you with credible contents